Mhe. Mchengerwa awaongoza watanzania kumpokea Gurudev Sri Sri Ravishankar
Na John Mapepele
Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa leo Agosti 25, 2022 amewaongoza watanzania kumpokea kiongozi mashuhuri duniani ambaye ni kiongozi wa kiroho na balozi wa amani duniani Gurudev Sri Sri Ravishankar.
Mara baada ya kuwasili uwanja wa ndege wa kimataifa wa Dar es Salaam amepokewa na Mhe Mchengerwa na Katibu Mkuu wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Dkt, Hassan Abbasi ambaye ni Mwenyekiti wa Kamagi ya Royal Tour.
Baada ya kuwasili Gurudev Sri Sri Ravishankar amesema amejisikia furaha kuja Tanzania kwa kuwa nchi ya amani.
Kiongozi huyo mwenye zaidi ya wafuasi milioni 500 atakuwa na ziara ya siku tatu nchini na anatarajiwa kufanya tukio la kiutamaduni kukutana na viongozi na kutembelea maeneo ya utalii.
Aidha leo jioni majira ya saa 12 atashiriki tukio la kihistoria la utamaduni wa India na Tanzania na kutoa mhadhara katika Kituo cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
Pia yeye na ujumbe wake wataangalia filamu ya Tanzania: The Royal Rour ambapo amepanga kutembelea mbuga za wanyama ikiwa ni mwitikio wa Rais Samia Suluhu Hassan katika kutangaza Tanzania kupitia filamu ya Royal Tour.
Mhe. Mchengerwa amemwelezea kiongozi huyo wa kiroho kuwa ni miongoni wa viongozi ambao Serikali ya Tanzania inawathamini Kwa mchango wake mkubwa wa kupigania amani duniani.
Ameongeza kuwa watanzania wamefarijika na ujio wake na kwamba wanamkaribisha kutembelea vivutio mbalimbali vya Utalii ili kujionea vivutio na utajiri wa utamaduni wa Tanzania.
Mara baada ya kutua kwenye uwanja wa ndege mgeni huyu amepokewa na kikundi cha Sanaa cha ngoma kutoka Bagamoyo ambapo alivutiwa nacho kiasi cha kumfanya kujumuika na kuanza kucheza na wasanii hao aisindikizwa na mwenyeji wake Mhe. Mchengerwa.






 
 
 
Comments
Post a Comment